Friday, March 13, 2009

WE MWALI, KAMLONGELE MWALI MWANA WA MWALI MWALI

Taarifa hii kwa wote watokao kijijini Nyambogo na Nzilimiti (Wilaya ya Morogoro Vijijini, mkoani Morogoro) wanakaribishwa na wengine pia kuchangia katika blogu hii. Hii maana yake ni kwamba Wazungumzao lugha ya Kiswahili wote mnakaribishwa mlioko duniani kote.

Nimeanzisha blogu hii kwa kumbukumbu tu ya kuzaliwa kwake Bw. Bwakilla Tariq Abdul Mlekwa Machi 15, 2003 katika Manispaa ya Morogoro, nchini Tanzania, Afrika Mashariki, barani Afrika.

Tafsiri ya maneno yaliyopo katika kichwa cha habari ni kama hivi:
Wee mwali, kamwambie mwali kuwa mwanawe mwali kawa mwali (yaani amevunja ungo). Usemi huu hutumika sana kwa watokao katika maeneo tajwa hivyo nimeona kwa jinsi ulivyo ni usemi wa shangilizi, niuweke katika blogu hii ili wasioufahamu usemi huu nao waufahamu. Hasa kwa sababu usemi huu asilia uko katika hatari ya kutoweka kwa sababu, siku hizi (katika karne hii ya 21) hatusherehekei tena galigali; ambayo ni sherehe ya kutaarifu jamii inayokuzunguka kuwa binti yako amevunja ungo.

Pia siku hizi mila za kucheza ngoma na kutayarisha Wakasano, Wannandi, na Wahunga Wakulu na Wadogo wote sasa yanapotea hasa kutokana na kusambaa zaidi kwa miji na kutoweka kwa vijiji na pia kutokana na umasikini uliokithiri vijijini. Vilevile tamaduni hizi zinatoweka kutokana na kuiga tamaduni nyingine duniani hasa zile zinazoletwa na tekinolojia ya kisasa kama televisheni, simu za mkononi, Ipod, Blueberries, na kadhalika.

Hivyo, mwenye jambo lolote lile la kiasili yake mwenyewe au alilolisikia, karibuni sana katika uwanja huu tuweke na kuhifadhi tamaduni zetu ili watoto, wajukuu, vilembwe na vitukuu vyetu vije kusoma tamaduni zetu zinazopotea. Hata ukiwa na nyimbo asilia pia karibu uziweke humu kwa ajili hiyo hiyo. Kwa upande wa nyimbo hata hivyo, ni muhimu kuzitafsiri katika Kiswahili ili wasiofahamu lugha ya wimbo huo nao wapate kufaidika kama nilivyotafsiri kichwa cha habari hiki cha kwanza katika blogu hii. NAWAKARIBISHA KWA MIKONO MIWILI, KARIBUNI.

No comments:

Post a Comment

BLOGU YA KUWEKA KUMBUKUMBU ZA ASILI ZA WATANZANIA, WAAFRIKA NA WOTE WAZUNGUMZAO LUGHA YA KISWAHILI DUNIANI.